Nunua hisa za Benki Tarajiwa ya Walimu kupitia Vodacom M-Pesa sasa…


Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Rosalynn Mworia (katikati),akifafanua jambo kwa waandishi wa habari (hawamo pichani) wakati wa kutangaza ushirikiano wa kimkakati na Benki Tarajiwa ya Walimu (Mwalimu Commercial Bank in-formation) kurahisisha ununuaji hisa kupitia huduma ya M-Pesa pamoja na kampuni ya Maxcom Africa kupitia huduma yake ya Maxmalipo, Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo Ronald Manongi na kulia ni Ofisa Mkuu wa Maswala ya Biashara wa Max Malipo Ahmed Lussasi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Mwalimu Commercial Bank (in-formation), Ronald Manongi na Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Rosalynn Mworia (kushoto) wakipeana mikono ikiwa ishara ya uzinduzi wa ushirikiano wa kimkakati na Benki hiyo kurahisisha ununuaji hisa kupitia huduma ya M-Pesa pamoja na kampuni ya Maxcom Africa kupitia huduma yake ya Max Malipo. Wengine katika picha wapili kushoto ni Ofisa Mkuu wa Maswala ya Biashara wa Max Malipo Ahmed Lussasi na Mwekahazina Mkuu wa Benki hiyo Nunu Saghaf.

Dar es Salaam, 22 Aprili, 2015 – Chama cha Walimu Tanzania (CWT) ambao ni waanzilishi wa Benki Tarajiwa ya Walimu (Mwalimu Commercial Bank in-formation), kinawatangazia Walimu na Watanzania wote kwa ujumla  juu ya uuzwaji wa Hisa za Benki tarajiwa ya Walimu, kwa lengo la kupanua wigo wa wanahisa na kuongeza mtaji ulianza tarehe 23 Machi 2015 na unategemea kumalizika tarehe 4 Mei 2015.

Ili kufikia azma hii, pamoja na njia nyingine za uuzaji wa Hisa zake, Benki Tarajiwa ya Walimu inatangaza ushirikiano wa kimkakati na kampuni ya mawasiliano ya Vodacom kupitia huduma yake ya M-Pesa pamoja na kampuni ya Maxcom Africa kupitia huduma yake ya Maxmalipo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa ushirikiano huu, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano wa Umma wa Vodacom Tanzania, Rosalynn Mworia alisema, “Tunafahamu umuhimu wa kuwezesha Walimu na Watanzania wote kununua hisa kwa urahisi kabisa bila kutoa mguu majumbani kwao na hivyo tumeamua kushirikiana na Benki Tarajiwa ya Walimu kurahisisha zoezi hili la ununuaji hisa kupitia huduma yetu ya M-Pesa inayopatikana nchini kote kupitia mtandao wa mawakala zaidi ya 85,000.”

Vodacom kupitia huduma yake ya M-Pesa imerahisisha ununuzi wa hisa kupitia simu za mkononi kwa kuondoa adha ya usajili. Mteja anapoingiza namba yake ya simu kama namba ya kumbukumbu moja kwa moja taarifa zake zinaingizwa kwenye rekodi kupitia mifumo ya Maxcom Africa.

Sasa hatua za usajili na manunuzi zimeunganishwa katika mchakato mmoja kupitia huduma hii ya M-Pesa.  Ili kufanya manunuzi ya hisa mteja anatakiwa kupiga *150*00# kupata menu ya M-Pesa na kisha kuchagua “Lipa Kwa M-Pesa” halafu achague Namba ya Kampuni na kisha ingiza 236622 kama Namba ya Kampuni. Hatua inyofuata ni kuingiza namba ya simu kama kumbukumbu ya malipo na kisha kiasi anacholipia kulingana na idadi ya hisa alizonunua. Hatua ya mwisho ni kuweka PIN ya M-Pesa na kisha Kamilisha Muamala.

Hisa moja itauzwa kwa shilingi mia tano tu (Tsh. 500/-) na kiwango cha chini cha manunuzi ya Hisa ni Hisa mia moja (100) sawa na shilingi elfu hamsini (Tsh. 50,000/-) na baada ya hapo unaweza kununua Hisa hizi kadri ya uwezo wako.

“Tulipozindua ununuzi wa hisa za Benki Tarajiwa ya Walimu mnamo Machi 23, 2015 tulitumia mfumo ambao ulihitaji mteja kujisajili kwanza kabla ya kununua hisa lakini sasa M-Pesa imerahisisha zoezi hili kwa kuondoa hatua ya usajili. Tunatumaini kuwa sasa tutaweza kupata idadi ya wanahisa wasiopungua laki tatu kama tulivyopanga hapo awali,” alisema Rais wa Chama cha Walimu Tanzania, Mwalimu Gratian Mukoba

“Tunawahakikishia Walimu na Watanzania wote kuwa huduma hii ni rahisi sana, ya uhakika na salama kabisa kama ambavyo miamala mingine inayopitia huduma ya M-Pesa ilivyo salama,” aliongeza.

Nia na madhumuni ya ushirikiano huu wa kihistoria ni kurahisisha uuzwaji wa Hisa za Benki Tarajiwa ya Walimu na kutoa fursa hii adimu kwa Walimu zaidi ya laki mbili na mamilioni ya Watanzania kumiliki Benki na hivyo kujumuishwa katika uchumi wa kisasa kwa nia ya kuboresha maisha yao.

Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) Bibi Nasama Massinda alisema kuwa juhudi za Mamlaka hiyo za kuwezesha wananchi wengi kushiriki katika masoko ya mitaji kwa kununua hisa zilikwama kwa muda mrefu kutokana na changamoto mbalimbali. 

Ushirikiano huu wa leo kati ya mwekezaji yaani Benki Tarajiwa ya Walimu na kampuni za Vodacom Tanzania na Maxcom Africa ni mafanikio makubwa yaliyotokana na ya utekelezaji wa utaratibu wa kuwezesha wawekezaji kushiriki katika masoko ya mitaji kwa kutumia teknolojia kupitia Miongozo ya Uuzaji na Ununuzi wa Hisa kwa Njia ya Teknolojia ya Mawasiliano (Capital Markets and Securities Electronic Trading Guidelines, 2015).

“Sasa mwalimu anaweza kununua hisa huku akiendelea kusahihisha madaftari ya wanafunzi katika kituo chake cha kazi popote alipo iwe mjini au kijijini. Kwa kuwa uuzaji wa hisa za benki tarajiwa ya Mwalimu uko wazi kwa watu wote, hivyo basi kwa mara ya kwanza katika nchi yetu wananchi wanaweza kununua hisa katika soko la awali kupitia teknolojia ya simu za mikononi.

“Haya ni mageuzi makubwa katika maendeleo ya masoko ya mitaji kwani, Mamlaka ya Masoko ya Mitaji ya Tanzania inaweka historia kwa kuwa Mamlaka ya kwanza katika nchi za ukanda wa Afrika ya Mashariki (EAC) kwa kuwezesha ununuzi wa hisa katika soko la awali (IPO) kwa kupitia simu za mkononi,’’ aliongeza.

Katika kuweka kwa vitendo yaliyozungumzwa hapo juu na viongozi hao, Benki Tarajiwa ya Walimu na Vodacom kwa kushirikiana na MaxMalipo kwa pamoja watafanya kampeni ya uhamasishaji wa uuzwaji wa Hisa za Benki Tarajiwa ya Walimu kupitia huduma ya M-Pesa ambayo imewezesha kuboreshwa zaidi kwa mchakato wa ununuzi wa Hisa ili kukidhi mahitaji ya wanunuzi. 

MaxMalipo watatoa msaada na huduma kwa wateja kwa saa 24 kupitia namba 0764 700 200.
Mbali na M-Pesa unaweza kununua Hisa za Benki Tarajiwa ya Walimu kupitia mawakala wa Maxmalipo wanaopatikana kote nchini na katika ofisi zote za posta, matawi yote ya Benki ya CRDB nchini na mawakala wote wa Soko la Hisa la Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment

Pages