MAWAKALA WA MAXMALIPO SASA KUTOA HUDUMA ZA BENKI YA CRDB


Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dk. Charles Kimei akibadilishana hati ya mkataba wa makubaliano na Mkurugenzi wa Maxcom Africa, Juma Rajabu baada ya uzinduzi wa huduma za ‘FahariHuduma wakala’ kupitia vituo vya Maximalipo. Hafla imefanyika leo jijini Dar es Salaam. (Picha na Francis Dande) 
 Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dk. Charles Kimei na Mkurugenzi wa Maxcom Africa, Juma Rajabu wakisaini hati ya mkataba wa makubaliano wa huduma za ‘FahariHuduma wakala’ kupitia vituo vya Maxmalipo. 
  Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, anayeshughulika na Uendeshaji na Huduma kwa Wateja, Saugata Bandyadhiyay akisaini hati ya mkataba wa makubaliano wa huduma za ‘FahariHuduma wakala’ kupitia vituo vya Maxmalipo.
  Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dk. Charles Kimei akifurahia jambo na Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, anayeshughulika na Uendeshaji na Huduma kwa Wateja, Saugata Bandyadhiyay.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Dk. Charles Kimei akizugumza wakati wa hafla hiyo.
 Baadhi ya Wakurugenzi wa Benki ya CRDB wakiwa katika hafla hiyo.
Picha ya pamoja.
BENKI ya CRDB na kampuni ya Maxcom Africa, imeingia mkataba wa makubaliano utakaowezesha wakala wa Maxmalipo kutoa huduma za benki hiyo kupitia mfumo wa fahari huduma.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa benki ya CRDB, Dk. Charles Kimei, alisema makubaliano waliyoyafikia yatasaidia benki hiyo kutumia mtandao wa mawakala wa maxmalipo kutoa huduma kwa wateja kiurahisi.

Alisema lengo la makubaliano hayo ni kupanua wigo wa kutoa huduma ili kuweza kuwafikia Watanzania wengi.

Alisema huduma hiyo itasaidia kuweka na kutoa fedha kwenye akaunti za wateja wa CRDB, kutuma fedha kwa watu wenye akaunti na wasio na akaunti za benki, kupokea fedha walizotumiwa na wateja, kupokea marejesho ya mikopo mbalimbali, kulipia Ankara, kuangalia salio na kuhamisha fedha kwenda kwenye akaunti nyingine ndani ya CRDB.

Dk. Kimei alisema ingawa huduma ya fahari kupata mafanikio kwa kipindi kifupi bado Watanzania wengi wako nje ya mfumo huo na kueleza kwamba ni asilimia 17 ya watanzania wote walio kwenye mfumo halali wa fedha.

Alisema kwamba kwasasa wana mawakala 1,500 wameshajiunga na kuanza kutoa huduma kwa wateja ambapo wastani wa miamala 300,000 hufanyika kila mwezi. 

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Maxcom Tanzania, Juma Rajabu, alisema ni fahari kwa kampuni yao kupata fursa ya kufanya kazi na CRDB na kuahidi kuendelea kujiimarisha ili kuweza kuwafikia Watanzania wengi.

No comments:

Post a Comment

Pages