WIZARA YA BIASHARA, VIWANDA NA MASOKO ZANZIBAR KUCHANGAMKIA FURSA ZA TADB



Katibu Mkuu wa Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko Zanzibar, Bw. Bakari H. Bakari (katikati) akiongoza kikao cha pamoja na Benki ya Maendeleo ya Kilimo ya Tanzania (TADB), kilichofanyika katika Makao Makuu ya Wizara hiyo.

Mjumbe wa Bodi ya TADB, Bibi Rehema Twalib ambaye ni Mkuu wa Msafara huo (wapili kulia) akizungumza wakati walipotembelea Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko Zanzibar. Kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko Zanzibar, Bw. Bakari H. Bakari.

Wajumbe wa kutokana TADB wakifuatilia kwa makini mazungumzo na uongozi wa Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko Zanzibar. Mazungumzo hayo yalifanyika katika Makao Makuu ya Wizara hiyo.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Bw. Francis Assenga (kulia) akieleza dhima ya Benki ya Kilimo katika kusaidia juhudi za Serikali katika kuinua ukuaji wa uchumi na kupunguza umaskini nchini.

Mkurugenzi wa Mikopo na Biashara wa TADB, Bw. Augustino Chacha (katikati) akizungumzia fursa za mikopo inayotolewa na Benki hiyo wakati walipotembelea na kufanya mazungumzo na viongozi wa Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko Zanzibar (hawapo pichani). Wengine pichani ni Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TADB, Bw. Francis Assenga (kulia) na Meneja wa Mikopo wa TADB, Bw. Samuel Mshote (kushoto).




Katibu Mkuu wa Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko Zanzibar, Bw. Bakari H. Bakari akihiimiza jambo wakati wa kikao cha pamoja na viongozi wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo ya Tanzania (TADB), kilichofanyika katika Makao Makuu ya Wizara hiyo.

Meneja wa Mikopo wa TADB, Bw. Samuel Mshote (kulia) akizungumza wakati wa kikao hicho.


Na Mwandishi wetu,
Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko Zanzibar imesema itakuwa ya mwanzo kuanza kutumia fursa za mikopo nafuu inayotolewa na Benki ya Maendeleo ya Kilimo ya Tanzania (TADB) ili kuchagiza uwekezaji katika sekta ya uchakataji wa mazao na masoko ili kuongeza tija kwa maendeleo visiwani Zanzibar.


Mkakati huo umewekwa bayana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Bw. Bakari H. Bakari wakati akizungumza na ugeni kutoka TADB uliomtembelea Ofisini kwake.


Bw. Bakari amesema kuwa ujio wa Benki hiyo unatoa fursa kubwa sana kwa sekta zilizo chini ya wizara yake ikiwamo biashara, viwanda na masoko.


“Tuna imani kubwa ujio wa TADB utatusaidia kutatua changamoto zinazozikabili sekta hizi ambazo zinakabili na changamoto ikiwemo ukosefu wa masoko ya mazao; ufinyu wa bei za mazao; miundo mbinu mibovu ya usafirishaji; maghala ya kuhifadhi mazao; nishati ya umeme na miundombinu hafifu vijijini; ufinyu au kutokuwepo kwa ongezeko la thamani kwa mazao ya kilimo; mabadiliko ya hali ya hewa; na mmomonyoko wa udongo,” alisema.


Akizungumza wakati wa mazungumzo hayo, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Bw. Francis Assenga alisema uanzishwaji wa TADB unatokana na Serikali kutambua umuhimu wa uwekezaji wenye tija kwenye maeneo yote ya sekta ya kilimo na kuleta mapinduzi ya dhati ya Kilimo ili kuwezesha upatikanaji wa mikopo na mitaji ya riba nafuu ikiwa ni pamoja na kuhamasisha mabenki na taasisi zingine za fedha nchini kutoa mikopo zaidi kwenye sekta ya Kilimo.


Bw. Assenga alisema visiwa vya Zanzibar vitaingizwa rasmi katika mpango wa biashara wa Benki na ametoa wito kwa wakulima na wafanyabiashara wa mazao ya kilimo visiwani humo kuchangamkia fursa zinazotolewa na TADB.

No comments:

Post a Comment

Pages