KIWANDA CHA GRANDE DEMAM CHAONGEZA THAMANI YA MAZIWA WILAYA YA ARUMERU


Na Woinde Shizza ,Arusha


WAKURUGENZI wa Kiwanda cha Grande Demam kilichopo wilayani Meru mkoani Arusha wameamua kuongeza thamani ya maziwa ya ng'ombe huku
wakihamasisha Watanzania kunywa maziwa yalisindikwa kwani hayana madhara kwa mlaji zaidi ya kumkinga na magonjwa yanayoweza kuambikizwa kutoka kwa wanyama kwenda kwa binadamu.


Uamuzi wa kuongeza thamani ya maziwa umetokana kiwanda hicho kuongeza wigo na kununua maziwa zaidi kwa wafugaji wilayani hapo ambao walikua wakiteseka kupata masoko na wakati mwingine kumwaga maziwa yao yanayoharibika kwa kukaa muda mrefu bila kununuliwa.


Imefahamika Wilaya ya Meru ni moja kati ya Wilaya maarufu zinazoongoza kwa uzalishaji mkubwa wa maziwa mkoani Arusha na maziwa hayo huuzwa maeneo ya miji ikiwemo viunga vya Jiji la Arusha na nje ya Jiji hilo.


Licha ya uzalishaji huo wa maziwa bado wafugaji hao wa wilaya hiyo ya Arumeru walikuwa wanakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa masoko ya uhakika ya kununua maziwa hayo, hivyo kusababisha kuharibika baada ya kukaa kwa muda mrefu bila kununuliwa.


Akizungumza leo mmoja wa wakurugenzi wa kiwanda hicho Dk.Deo ambaye ni mtaalam wa mifugo anasema kutokana na changamoto hiyo kwao wakaifanya kuwa fursa ya wao kuwekeza kiwanda cha kusindika maziwa.


Dk.Deo anasema kwa kuwa wafugaji hao walikua wakiyamwaga maziwa yao yaliyokuwa yakiharibika kwa kukosa soko la uhakika na hawakuwa na namna yoyote ya kuongeza thamani maziwa hayo ili yaweze kukaa kwa muda bila kuharibika baada ya kuanzisha kiwanda hicho imesaidia kuongeza thamani ya maziwa.


Anafafanua aliamua kuacha kazi mwaka 2001 na kuamua kufuga ng'ombe mmoja na baadae wakaongezeka kuwa wawili ambao walikuwa wanatoa lita 40 kila siku huku yeye na familia yake wakitumia lita moja,hivyo maziwa mengine yalikuwa yanaharibika.


"Hali hiyo ilinafanya nimtafute mtaalam kutoka Kenya ambaye atafundisha jinsi ya kuongeza thamani ya maziwa ya ng'ombe kwa kuyafungasha na kuyauza. Mtaalamu huyo alinifundisha na ndipo nilipoanza kuongeza thamani ya maziwa.


"Baada ya muda ya muda majirani zangu ambao ni wafugaji walianza kuvutiwa na jinsi ninavyoongeza thamani ya maziwa yake.Hivyo nao wakaanza kunufaika kwani nilianza kwa kununua lita 100, baadae nikawa nanunua lita 150 na sasa nanunua lita 200 kwa siku,"amesema Dk.Deo.
Anasema baada ya hapo akafungua kiwanda kidogo ambacho kilikua na uwezo wa kusindika lita 200 kwa siku huku wafugaji wakimpelekea maziwa zaidi ya hapo ndipo alipoongeza uzalishaji na sasa kwa siku anazalisha lita 2000.


Dk.Deo anasema kutokana na ongezeko hilo la uzalishaji ,wakurugenzi wenzake wa kiwanda hicho cha The Grande Demam wameongeza wigo na kununua maziwa zaidi kwa wafugaji ambao walikua wakiteseka kupata
masoko na wakati mwingine kumwaga maziwa yao yanayoharibika.


Amefafanua kiwanda hicho kinanunua maziwa bora kutoka kwa wafugaji na kuyaongezea thamani ikiwa ni pamoja na kuyafungasha vyema.
"Maziwa ambayo hayajaongezwa thamani hukaa kwa muda wa saa 13 lakini maziwa yaliyoongezwa thamani yanakaa hadi mwezi mmoja jambo linalota unafuu hasa kwa kipindi kifupi kabla hayajafika sokoni".


Dk.Deo anaeleza maziwa yaliyosindwa ni mazuri kwa afya ya binadamu kwani yanakuwa yameondolewa bakteria na kuongezewa bakteria rafiki kwa afya.Mtu anayetumia maziwa yasiyosindikwa anakuwa na hatari ya kupata magonjwa mbalimbali ikiwemo TB, yphoid na Brusela.


Dk.Deo anasema maziwa ni bidhaa yenye faida kubwa katika mwili wa binadamu ikiwemo virutubisho aina ya protini,madini,fat na wanga na kufafanua unywaji wa maziwa uhamasishwe kwa wingi katika jamii ili kuwa na jamii yenye afya bora inayoweza kushiriki shughuli za uzalishaji.


"Tuna mpango wa kuzalisha mpaka lita 100,000 kwa siku na uzalishaji huu
utaleta tija kwa kiwanda na wafugaji ambao tumekua tukinunua maziwa
kwao.Tutanunua maziwa mengi zaidi na hivyo tutaongeza kipato cha mfugaji ambao watanufaika na shughuli zao,"amesema Dk.Deo.


Amesema ni vema Watanzania wakajifunza kunywa maziwa haya bora yanayozalishwa nchini badala ya kunywa maziwa kutoka nje kwani kwa kufanya hivyo utakua unainua uchumi wa nje.


Dk.Deo amesema biashara ya maziwa imesaidia vijana wengi waliojiriwa na kiwanda hicho katika sekta ya uzalishaji na usambazaji jambo ambalo linaonesha mnyororo wa wanufaika wa kiwanda hicho unavyoongezeka."Kwa sasa bidhaa za maziwa,Yogat na Siagi za The Grande Demam imefika katika mikoa ya Dar es Salaam ,Manyara ,Tanga na Morogoro,"amesisitiza.


Kwa upande wa Mshauri wa Masuala ya Biashara katika kiwanda hicho Peter Ojukwu amesema kiwanda kimesaidia kunufaisha wananchi zaidi ya 4500 kutokana na mzunguko wa uzalishaji mpaka kumfikia mlaji.


"Licha ya kiwanda hicho kujikita na uzalishaji wa maziwa bado tunatoa huduma za ushauri wa ufugaji bora,matibabu ya mifugo na dawa ili waweze kufanya ufugaji wenye tija,"amesema.
Baadhi ya Wafanyakazi na Viongozi wa Kiwanda cha Maziwa cha The Grande Demam wakihakiki ufungashaji wa bidhaa za maziwa zinazozalishwa kiwandani hapo
Baadhi ya Viongozi wa kiwanda cha maziwa cha The Grande Demam wakinywa maziwa yanayozalishwa na kiwanda hichoBaadhi ya Viongozi wa kiwanda cha maziwa cha The Grande Demam wakinywa maziwa yanayozalishwa na kiwanda hicho


Uongozi wa kiwanda cha maziwa cha The Grande Demam

No comments:

Post a Comment

Pages